Advertisements

Thursday, August 28, 2014

Buriani BETTY NDEJEMBI: Tusake #JusticeFor Betty kwa kupambana na unyanyasaji mtandaoni (Cyberbullying) pia

Ninaandika makala hii nikitambua bayana kuwa itamuudhi kila mtu anayeingia mtandaoni kwa minajili ya kuwanyanyasa watu wengine. Lakini siku zote ninaamini katika busara hii: kuuchukia ukweli hakuufanyi kuwa uongo. Ukweli ni ukweli na uongo ni uongo. Ukweli hauwezi kuwa uongo, na kadhalika uongo hauwezi kuwa ukweli. Kamwe asilani.
Wakati tunaomboleza kifo cha ndugu yetu Betty Ndejembi hatuwezi kukwepa ukweli kwamba siku chache kabla ya kifo chake binti huyo alinynyaswa mno kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter. Japo hadi muda huu hatuwezi kuhusisha moja kwa moja uhusiano kati ya unyanyasaji huo na kifo cha binti huyo, ukweli tu kwamba mtu akinyanyaswa masaa kadhaa kabla ya kifo chake, waweza kujenga picha flani.
Naomba ieleweke kuwa simlaumu mtu kwa sababu sina mamlaka ya kufanya hivyo bali dhima ya makala hii ni rambirambi zangu na kuzungumzia tatizo la unyanyasaji mtandaoni, sambamba na suala zima la unafiki kila kinapojiri kifo hususan cha mtu maarufu.
Tuna tatizo kubwa huko mitandaoni. Tumefika hatua ya kuwapa umaarufu watu wenye matusi ya nguoni, wazushi, wambeya, wanafiki, wanaharamu na kila aina ya binaadamu wanaostahili laana lakini twaishia kuwatukuza. Kwa Twitter, matusi imekuwa ni njia ya mkato ya kupata umaarufu. Kuna wenzetu wengi tu wenye 'umaarufu' huko Twitter, na ukidadisi chanzo cha 'umaarufu' huo, utaambiwa 'ah huyu ana matusi si mchezo!'
Kuna watu wazima na akili zao wanatumia muda mwingi kwenye mitandao ya kijamii aidha kunyanyasa wenzao kama si kusherehesha unyanyasaji huo. Marehemu aliitwa majina kadhaa ya kumdhihaki kabla ya kukutana na mauti. Kuna waliomwita Di Maria na wanajifahamu. Japo sijui chanzo cha 'ugomvi na aliogombana nao' (na ndio maana sikujihusisha nao kwani haukunihusu), kuna wanafiki wengi tu waliokuwa katika nafasi nzuri ya kuzima moto huo hasa kwa vile baadhi yao walikuwa wakizifahamu pande zote mbili za 'ugomvi' husika.
La kukera zaidi ambalo ni wazi litajichomoza wakati wa maombolezo haya ni unafiki: baadhi ya watu walewale waliodiriki kumwandama marehemu wakati wa uhai wake watageuka kuwa wenye uchungu mkubwa baada ya kifo chake. Hii inanikumbusha suala ambalo nimeshawahi kulizungumzia mara kadhaa, katika hali ya utani japo wenye uweli, kwamba 'wakati mwafaka kabisa wa kutafuta vipaji vya uigizaji ni kwenye misiba: watu walewale waliokuwa wakikuchukia kwa nguvu zote watageuka wenye uchungu mkubwa kwa kifo chako.
Ukiangalia baadhi ya tweets za mwisho za marehemu ni wazi kuwa binti huyo alikuwa anahitaji msaada kutoka kwa wanaomjali
Hata pasi uelewa wa taaluma ya saikolojia, tweets za aina hii zinaashiria tatizo, na laiti 'wenye upendo wa dhati' wangeingilia kati muda huo, huenda muda huu Betty asingekuwa marehemu. 
Na hizo tweets mbili ambazo ni miongoni mwa za mwisho kabisa za marehemu ni ushuhuda tosha wa jinsi alivyokuwa akisumbuliwa na wanyanyasaji dhidi yake mtandaoni. Ndio pengine kilichomuua ni maradhi ya kawaida ya kibinadamu lakini kila mwenye ubinadamu hatoshindwa kuhusisha unyanyasaji huu na hali mbaya ya afya aliyokuwa nayo hadi anafariki.
Kuna watakaolaumu kuwa ninatumia kifo cha binti huyo kwa 'maslahi binafsi.' Hapana, sina maslahi yoyote binafsi hasa ikizingatiwa kuwa sikuwa nikifahamiana na marehemu. Hakuna anani-follow na mie sikuwa nam-follow. Labda maslahi pekee niliyonayo ni upinzani wangu mkali dhidi ya unyanyasaji wa mtandaoni. Vyovyote ilivyo, marehemu alikuwa bullied kabla hajafariki na atakayetaka kukataa ukweli huo na akatae lakini utabaki kuwa ukweli usioweza kugeuka uongo. Na kwa hakika, kila aliyeshiriki kumnyanyasa binti huyo atakuwa anasutwa na nafsi yake, hata kama atatafuta hifadhi kwenye 'huu sio wakati wa kulaumiana' au 'we failed you Betty.' 
Mara nyingi nimekuwa nikiwalaumu watu wanaodai 'Instagram imekuwa mbaya' au Twitter imeharibika siku hizi' ambapo mara zote nimewakumbusha wahusika kuwa katika hii mitandao ya kijamii, ni muhimu kuwa makini katika nani wa kum-follow. Maana yangu ni kwamba ukim-follow mtu mwenye matusi, utashuhudia matusi katika anachoandika. Ukim-follow mtu wa busara, utashuhudia busara.
Hata hivyo, katika siku za hivi karibuni kumeibuka kundi kubwa tu la watu wenye busara na elimu zao lakini wepesi wa kuvutiwa na vitu vya 'kipuuzi' - umbeya, matusi, majungu, na upuuzi mwingine, na hawasiti kushea na wanaowa-follow. Ni hivi, mtu akitweet tusi, kisha ukali-retweet, utambue kuwa unalikuza (amplify) tusi hilo. Na kimsingi, kwa kiasi kikubwa, tuna-RT vitu tunavyoviunga mkono. Uki-RT tusi maana yake unaliunga mkono. Na ni wazi mwenye kujiheshimu, na kuheshimu 'watu wa maana' wanaom-follow hawezi ku-RT upuuzi.
Tatizo kubwa sasa ni kwamba waweza kuamua kuwa-follow watu unaodhani wana busara au akili za kutosha lakini ukaishia kusoma vitu vya ajabu ajabu kwenye timeline yako kutokana na haya 'mahaba' ya ku-RT vitu vya kipuuzi. 
Binafsi, nadhani chanzo kikubwa cha mitandao ya kijamii kuwa 'sehemu za kukera, kuogopesha, kunyanyasana, nk' ni ile hali ya baadhi ya wenzetu kutokuwa na vitu muhimu vya kufanya katika maisha yao. Ni wazi kwamba ukiwa busy na maisha yako hutokuwa na muda wa kubughudhi wenzako.
Kingine kinachopelekea social media kuwa 'dunia uwanja wa fujo' ni ugonjwa mkubwa unawasumbua baadhi ya wenzetu: kusaka sifa wasizostahili. Wanasema,. ashakum si matusi, 'lugha ya mpumbavu ni matusi,' na ndo maana baadhi ya wenzetu wasio na cha maana cha kuongea katika hadhara hukimbili matusi, unyanyasaji, maneno macha
Nitamke bayana kuwa siandiki makala hii nikitegemea kuungwa mkono na wahusika wa unyanyasaji mtandaoni. Na kwa hakika kuna uwezekano mkubwa wa makala hii kuzua 'kampeni ya chuki' dhidi yangu kutokana na makala hii. Tatizo kubwa la wenzetu hawa ni kutotaka kuambiwa kuwa 'Hapana, hili ni kosa. Na kosa ni kosa, haliwezi kuwa sahihi.' Lakini pamoja na uwezekano wa 'kuwashiwa moto' kutokana na makala hii, wito wangu kwa kila mwenye busara na akili ni kuliangalia tukio hili la kusikitisha kama 'wake up call.' Tujifunze, tujisahihishe. Tuache kusherehesha vitu vya kipuuzi mtandaoni.
Ifike mahala, ukishindwa kumkemea mtu mwenye tabia mbaya mtandaoni basi chukua option rahisi ya kum-unfollow au ikibidi kum-block. Na ifike mahala kuwafahamisha watu wanaoendekeza utoto, majungu, umbeya, unyanyasaji na upuuzi mwingine kuwa kama hawana kitu cha maana cha kufany katika maisha yao basi isiwe sababu ya kuwasumbua wenzao wenye majukumu katika maisha yao.
Tukemee maovu badala ya kutarajia yataondoka yenyewe tu. Tuomboleze kifo cha Betty kwa kusema 'NO' kwa cyberbullies (wanyanyasaji wa mtandaoni). Tufike sehemu tuache kuwasujudia wahuni wanaodhani matusi ni sehemu ya wimbo wa taifa. Tuwakwepe waendekeza majungu, wanyanyasaji, wataka sifa za kipuuzi, na watu wasiofaa katik maisha yetu.
Wakati 'tunatafuta haki kwa marehemu Betty kutokana na unyama aliofanyiwa,' suala ambalo ni la kisheria, kilicho ndani ya uwezo wetu ni kukemea unyanyasaji mtandaoni (cyber bullying). Wakati hadi muda huu hatuwajui waliomfanyia marehemu unyama huo, takriban sote twawajua vema wanyanyasaji wa mtandaoni. Tuanze na hawa, kwani leo wamefanya kwa kwa marehemu Betty kesho itakuwa kwako.
Mwisho kabisa, ni muhimu kwetu sote kutambua kuwa tulitoka kwa udongo na tutarudi kwa udongo. Kifo ni hatma ya kila mmoja wetu.Betty ametutoka lakini nasi twaelekea huko. Visa, chuki, kunyanyasana, na vitu vingine visivyopendeza japo ni kama sehemu ya maisha yetu havipaswi kupewa nafasi katika maisha yetu haya ambayo hakuna mmoja wetu mwenye japo 'lue' ya lini yatafikia kikomo. TUPENDANE na TUHESHIMIANE.
Kwako marehemu Betty, hakuna tunaloweza kusema au kufanya sasa kurejesha uhai wako. Na hakuna neno sahihi la kuonyesha jinsi gani kifo chako kimewagusa wengi. Kubwa tunaloweza kufanya ni kukuombea kwa Mwenyezi Mungu akupatie pumziko la milele na mwanga wa milele akuangazie upumzike kwa amani. Amina.

2 comments:

Unknown said...

Asante kaka, umetupa soma jema, R.I.P Betty

Anonymous said...

Hi, ila kwa tusiojihusisha na mitandao ya kijamii au tusiomfahamu marehemu hatujaelewa unyama gani kafanyiwa hadi amekutwa na umauti