Advertisements

Thursday, June 23, 2016

ABAKWA, ATOBOLEWA MACHO, AFA

Mwili wa marehemu ukitolewa eneo la tukio.

Richard Bukos na Issa Mnally, AMANI

DAR ES SALAAM: Huu ni ukatili namba moja! Mwili wa mrembo ambaye jina lake halikuweza kupatikana mara moja umekutwa mtupu kwenye nyumba iliyohamwa na kuanza kuchakaa ‘pagale’, maeneo ya Manzese Uzuri, Dar baada ya kudaiwa kubakwa na kutobolewa macho, Amani linakupa zaidi.

Mwili wa mrembo huyo uligundulika asubuhi ya Ijumaa ya Juni 17, mwaka huu ukielea kwenye nyumba hiyo ambayo inadaiwa mmiliki wake aliihama kufuatia kujaa maji wakati wote hata baada ya mvua kukatika.

Amani lilifika eneo la tukio na kuukuta mwili huo ukielea kwenye maji yaliyojaa ndani ya nyumba hiyo huku umati ukihangaika kutaka kuutambua.
Amani likiwa miongoni mwa watu waliofika kushuhudia, askari wa Kituo cha Polisi Urafiki-Ubungo, wakifika eneo la tukio na gari aina ya Toyota Land Cruiser yenye namba za usajili PT 1902 na kuuchukua mwili huo kwa ajili ya kwenda kuufanyia uchunguzi.

Likiwa eneo la tukio gazeti lilizungumza na wakazi wa eneo hilo ambapo mkazi mmoja aliyekataa kutaja jina lake alisema mrembo huyo inaonekana alifanyiwa ukatili huo sehemu nyingine na kwenda kutupwa eneo hilo.

Jirani huyo alisema anahisi hivyo kwakuwa kama angefanyiwa ukatili huo eneo hilo ni lazima wangesikia kelele ambazo zingewashtua na kwenda kutoa msaada.

“Huyu itakuwa wamemfanyia ukatili huo huko na kuamua kuja kumtupa huku mabondeni ili kupoteza ushahidi lakini kama wangemfanyizia maeneo haya lazima tungesikia kelele,” alisema jirani huyo.
Jumba ulimokutwa mwili wa marehemu.

Gazeti hili katika udodosi wa tukio hilo lilizungumza na mjumbe wa nyumba kumi wa eneo hilo aliyejitambulisha kwa jina la Bibi Moza ambaye alisema akiwa kwenye pilika zake alipewa taarifa za tukio hilo.

“Baada kupata taarifa hizo haraka nilikimbilia eneo la tukio kuushuhudia mwili wa marehemu na kuwauliza wananchi wangu kama kuna mtu anayemfahamu marehemu lakini hakuna aliyemtambua.

“Ukweli haya mauaji yanatisha sana dada wa watu sijui kawakosea nini maskini ya Mungu, lakini nahisi itakuwa ni visasi na marehemu atakuwa anawajua waliomfanyia ukatili huu ndiyo maana walimtoboa macho kisha kumuua kabisa,” alisema mjumbe huyo.

Mashuhuda

Kufuatia tukio hilo, gazeti hili lilizungumza na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, ACP Christopher Fuime ambaye alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema juhudi za kuwasaka watuhumiwa zinaendelea.

“Hilo tukio limenifikia na tuko mbioni kuwanasa watuhumiwa wa mauaji hayo ya kinyama ili tuwafikishe mbele ya sheria,” alisema kamanda huyo.

GPL

No comments: